Monday, December 19, 2016

KUGEUKIA UKUTANI SEHEMU YA PILI

Mwandishi: Anderson Leng'oko

Utangulizi
Mpendwa msomaji; tulijifunza toka katika sehemu ya kwanza kuwa zipo faida nyingi za kuwa na mahusiano binafsi na Mungu. Tunaendelea na faida hizo. Lengo la kuzijadili faida hizi ni kuwafanya watu wawe na uwezo wa kuwasiliana na Mungu muda wote na wamjue Mungu binafsi. Lengo kuu ni kuwafanya watu kuwa na uhusiano binafsi na Mungu na wamweke Mungu mbele na karibu nao kuliko mtu mwingine yeyote. Baada ya kulisoma somo hili Mungu akusaidie kukuza mahusiano yako binafsi na Mungu ili uweze kumgeukia yeye katika kila changamoto unayokutana nayo.

Faida za kuwa na mahusiano binafsi na Mungu (zinaendelea)
Kuepuka kukatishwa tamaa
Watu unaowatafuta wakuombee na kuwashirikisha shida zako wanaweza kukukatisha tamaa kutokana na kuwa hawana mzigo na hawayaoni maumivu halisi unayopata kulingana na uzito ulionao katika shida husika. Kwa hivyo namna watakayokuhudumia inaweza isiwe ya kutosha kuliondoa tatizo lako. Yesu alikuwa anaomba na wanafunzi wake, lakini kutokana na jinsi walivyokuwa hawajui ni namna gani wangeweza kumsaidia au kumtia nguvu, walijikuta wanalala katika wakati ambao Yesu alikuwa anahitaji sana msaada wao. Kwa hivyo Yesu, kama asingekuwa na mahusiano binafsi na Mungu akawa anawategemea wanafunzi wake kama kiunganisho kati ya yeye na Mungu, basi ingekuwa shida sana kwake.

Mathayo 26:37-45
Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka.
Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami.
Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.
Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja?
Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu.
Akaenda tena mara ya pili, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwa haiwezekani kikombe hiki kiniepuke nisipokunywa, mapenzi yako yatimizwe.
Akaja tena, akawakuta wamelala; maana macho yao yamekuwa mazito.
Akawaacha tena, akaenda, akaomba mara ya tatu, akisema maneno yale yale.
Kisha akawajia wanafunzi wake, akawaambia, Laleni sasa, mpumzike tazama, saa imekaribia, na Mwana wa Adamu anatiwa katika mikono ya wenye dhambi.

Kipo kisa kimoja mimi kilinitokea miaka kadhaa iliyopita. Baada ya mama yangu mzazi kuugua Kansa kwa muda mrefu alifariki. Alipokuwa amefariki mimi nilienda kwenye mazishi yake pamoja na wenzangu, wa Fimbo ya Musa. Tulipofika mazishini dada yake mama yaani mama mkubwa tulimkuta akiwa anaumwa sana, ugonjwa wa kutisha ambao ulikuwa umepelekea hadi akili zake kuyumba. Alikuwa hawezi kusimama kwenye jua hata kwa dakika tano.


Sasa kwa kuwa mimi nilikuwa nimesema na Mungu kwa muda mrefu sana kuhusu ugonjwa wake huu, nilifurahia sana hatua ya Fimbo ya Musa ministry kuwepo pale kwani ilikuwa ni fursa nzuri sana ya kumuombea mama huyu.

Sasa baada ya kuwa tumeamua kumuombea mama mkubwa wangu tulienda kanisani ambako tulikuta viongozi wa kanisa ambao waliamua kutusaidia kuomba. Tulipokuwa tumeomba kwa muda mfupi kiongozi wa kanisa alianza kukatisha maombi ili afunge kipindi tuondoke. Hii ilitokea kwa sababu alikuwa hajui hasa mimi nilikuwa na mzigo kiasi gani juu ya huyu mama.

Nilikuwa nimemlilia Mungu kwa takribani mwaka mzima sasa kuhusu mama huyu kwani tatizo lake hilo lilikuwa limemsumbua kwa muda mrefu. Sasa hapa nilikuwa nimewasihi wana Fimbo ya Musa wanisaidie kuomba usiku huu kwani wao walitaka waondoke mara tu baada ya mazishi. Lakini nilipowaomba wabaki tumuombee mama mkubwa walikubali hivyo tukaamua tukafanye maombi. Sasa haiwezekani maombezi yaliyosababisha watu wakatishe safari yakaombwa kwa dakika kumi.

Sisemi kwamba maombi lazima yawe ya muda mrefu ili yajibiwe, ninachotaka hapa kusema ni kwamba siku ile mzigo niliokuwa nao mimi juu ya maombezi yale ulikuwa ni mkubwa sana hadi nilikuwa niko tayari hata kukesha kama mama mkubwa asingefunguliwa. Ni siku ambayo sitaisahau katika maisha yangu kwani Mungu alinipa nguvu ya ajabu sana kiasi kwamba nikaweza kwenda kufanya huduma nikiwa nimetoka kumzika mama yangu mzazi saa moja au mawili yaliyopita.

Hili lilikuwa ni jambo kubwa sana kwangu, kwani miezi mitatu iliyopita kabla ya hapo nilikuwa nimeoneshwa maono nikimuombea mama Mkubwa na siku hiyo tulipokuwa tunamuombea ilitokea ikawa vilevile kama nilivyoona kwenye maono na ilikuwa ni utimilivu wa yale maono kunihakikishia kwamba yale mambo tulikuwa hatuyafanyi kwa utashi wetu. Hivyo isingekuwa rahisi kwetu kuacha maombi eti tu kwa sababu kiongozi wa kanisa ameamua kuahirisha maombi ili awahi kwenye mkesha kule msibani (ambako ni kwetu).

Tulimwambia yule kiongozi wa kanisa kwamba kama walikuwa na haraka waende, na kweli tuliwaruhusu tukaendelea na maombi hadi mama mkubwa alipofunguliwa. Hii ndiyo faida ya kuwa na mahusiano binafsi na Mungu. Hautegemei mtu mwingine katika kuyashughulikia mambo yako. Unapokea amri kutoka juu na ni Mungu peke yake anayeweza kukwambia jambo ukalifuata na yeye uwe na hakika kwamba hatakuacha kamwe kwani ni rafiki yako wa karibu kuliko mtu mwingine yeyote hapa duniani.

Kwa hiyo kwenye mfano wa hapo juu tumeona kuwa tulikuwa na mzigo wetu binafsi na tulikuwa na nguvu za Mungu za kwetu ndani yetu, hatukuwa tunategemea viongozi wa kanisa, na kusema kweli hata tulipokuwa tunaanza kuomba pamoja nao tulitamani watupishe toka mwanzo; Haleluya!

Uwezo wa kukutana na Mungu moja kwa moja kama wewe, wala siyo kwa kupitia kwa mtu mwingine

Katika biblia kuna mifano ya watu kadha wa kadha waliotumia watu kumtafuta Mungu. Wana wa Israeli walimtumia Samweli kumtafuta au kukutana na Mungu, matokeo yake Samweli alipokaribia kufa walijawa na hofu kubwa na wakajikuta wanaomba mfalme; jambo ambalo Mungu hakulipenda hata kidogo.

1 Samuel 8:1-22
Hata Samweli alipokuwa mzee, aliwafanya wanawe wawe waamuzi juu ya Israeli.
Na jina la mwanawe mzaliwa wa kwanza aliitwa Yoeli; na jina la wa pili Abiya; walikuwa waamuzi katika Beer-sheba.
Ila wanawe hawakuenda katika njia zake, bali waliziacha, ili wapate faida; wakapokea rushwa, na kupotosha hukumu.
Ndipo wazee wote wa Israeli wakakutana pamoja, wakamwendea Samweli huko Rama;
wakamwambia, Angalia, wewe umekuwa mzee, na wanao hawaendi katika njia zako; basi, tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote.
Lakini neno hilo likawa baya machoni pa Samweli, waliposema, Tupe mfalme atuamue. Naye Samweli akamwomba Bwana.
Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti ya watu hawa katika kila neno watakalokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao.
Kwa kadiri ya matendo yote waliyonitenda tokea siku ile nilipowatoa katika Misri hata leo, kwa kuniacha mimi, na kwa kutumikia miungu mingine, ndivyo wanavyokutenda wewe.
Basi sasa, isikilize sauti yao; walakini, uwaonye sana, na kuwaonyesha desturi ya mfalme atakayewamiliki.
Naye Samweli akawaambia wale watu waliotaka mfalme maneno yote ya Bwana.
Akasema, Mfalme atakayewamiliki ninyi atakuwa na desturi hii; atatwaa wana wenu na kuwaweka kwake, kwa magari yake, na kuwa wapanda farasi wake; nao watapiga mbio mbele ya magari yake.
Naye atawaweka kwake kuwa maakida juu ya elfu, na maakida juu ya hamsini; na wengine atawaweka walime shamba lake, na kuvuna mavuno yake, na kufanyiza zana zake za vita, na vyombo vya magari yake.
Na binti zenu atawatwaa kuwa wafanyaji wa marhamu, na wapishi, na waokaji.
Atatwaa makonde yenu, na mashamba yenu ya mizabibu, na ya mizeituni, yale yaliyo mazuri sana, ili awape watumishi wake.
Naye atawatoza ushuru wa mbegu zenu na wa mizabibu yenu, awape maakida wake, na watumishi Wake.
Atawatwaa watumishi wenu na wajakazi wenu, na ng'ombe zenu walio wazuri sana, na punda zenu, naye atawatia katika kazi zake mwenyewe.
Atawatoza fungu la kumi la makundi yenu; nanyi mtakuwa watumwa wake.
Nanyi mtalia siku ile kwa sababu ya mfalme wenu mliyejichagulia; Bwana asiwajibu siku ile.
Walakini hao watu wakakataa kuisikiliza sauti ya Samweli; wakasema, Sivyo hivyo; lakini tunataka kuwa na mfalme juu yetu;
ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu.
Samweli akayasikia maneno yote ya watu, akayanena masikioni mwa Bwana.
Bwana akamwambia Samweli, Isikilize sauti yao, ukawafanyie mfalme. Kisha Samweli akawaambia watu wa Israeli, Enendeni kila mtu mjini kwake.

Samweli aliwatawala wana wa Israeli na alikuwa ni nabii juu yao. Lakini kutokana na kuwa wana wa Israeli walimtumia Samweli kukutana na Mungu, walijawa na hofu walipoona Samweli anakaribia kufa kwani walijua kwamba hawangekuwa na mtu ambaye angekuwa anawasiliana moja kwa moja na Mungu Samweli akishakufa. Huu ni udhaifu waliokuwa nao hawa wana wa Israeli, wangekuwa wamemjua Mungu ipasavyo na wana mahusiano binafsi na Mungu kila mmoja wao, basi wangekuwa na Roho wa Mungu ambaye angekuwa amewafunulia makusudi ya Mungu juu ya jambo hili na wangefuata mashauri ya Mungu badala ya kung’ang’ania mfalme.

Unapokuwa una mtu unayemtegemea akupeleke mbele za Mungu utayumba sana kiroho kwani huyu mtu akifa au akikuchoka hauna namna ya kuwasiliana na Mungu moja kwa moja.
Mungu akiishi na wewe atakuwa na mambo anayotaka uyafanye wewe kama wewe kwa kufuata mashauri yake. Wala hautafanya kwa kufuata wengine, kama Waisraeli wanavyosema kwamba tupe mfalme kama ambavyo wenzetu wengine wana mfalme.


Sikatai kwamba Mungu huwa anatumia watu kukutana na sisi muda mwingine; ninachotaka ujue hapa ni kwamba unatakiwa kuwa na mahusiano na Mungu ya moja kwa moja licha ya kuwa kuna watu ambao Mungu anaweza kuamua kuwatumia.

Usikose sehemu ijayo ili tupate nafasi ya kuliangalia suala hili kwa kina zaidi… wakaribishe na wengine wajifunze kutoka kwa Roho wa Bwana katika somo hili.


No comments:

Post a Comment