Tuesday, August 23, 2016

KWA HABARI YA ZINAA (SEHEMU YA KWANZA)


Mwandishi: Anderson Leng'oko

UTANGULIZI
Mada hii ni mada inayoogopwa na watu wengi au tuseme labda inazuiwa na watu wengi. Pia kanisa halijihusishi sana na kuliongelea suala hili, lakini biblia inatuhimiza kufundisha ili watu waimarike katika kweli yote.

Walengwa wa somo hili ni watu wote, waliookoka na hata wasiookoka, watu wa dini zote na madhehebu yote, watu wa kila rika na kila imani. Inafaa sana kuyasoma mambo haya kwa kila mtu. Kama una rafiki yako ambaye hajalisoma somo hili tafadhali sana mpe alisome bila kujali imani yake, tabia zake, wala rika lake. Ujumbe huu unatakiwa kusikika kwa kila mwenye uhai hivyo ukibahatika kuusoma usikae nao, mwambie na mwenzio ausome.

Somo hili linatolewa kwa lengo la kujenga, maneno yaliyotumiwa au mambo yaliyoelezewa yanatumika kwa ajili ya kulijenga kanisa na si vinginevyo. Muda mwingi sana umetumika kuandaa somo hili. Roho Mtakatifu amekuwa akitoa vitu vingi karibu kila siku vya kuongezea hata ikaonekana dhahiri kuwa kama somo hili lisipoanza kutolewa ili kulisubiri liishe, yumkini halitaisha.

Kwa wakati huu nakupa sehemu ya kwanza ya somo hili lakini sehemu nyingine zitaendelea kukujia ambazo nazo zina ujumbe muhimu sana kwako kama kanisa la Kristo. Mungu akikujalia kuyasoma maneno haya na kuyatumia vizuri hakika yake utashinda kila changamoto unayokutana nayo kuhusu zinaa katika maisha yako.

Natumaini na kumuomba Mungu kuwa kila neno lililoandikwa katika somo hili litakufaa kwa kuyajenga maisha yako katika roho na kukuimarisha hata uzima wa milele.


ZINAA NI NINI?
Katika biblia zinaa inatumiwa kumaanisha tendo la kufanya mapenzi na mtu asiyekuwa mkeo wala mumeo, ukiwa tayari mwanandoa. Lakini katika somo hili tutatumia neno la zinaa kumaanisha kufanya mapenzi isivyo halali kwa ujumla, ambapo kuna wakati neno zinaa litatumika kumaanisha uasherati, yaani kufanya mapenzi kabla ya ndoa, kuna wakati litatumika kumaanisha pia tendo la kufanya mapenzi na mtu asiye mumeo wala mkeo wakati wewe umeoa au umeolewa.

FURAHA YENYE GHARAMA KUBWA
Hapa duniani, kila jambo la kufurahisha lina gharama zake. Kwa mfano, kunywa maji huleta raha kwa mwili, maji haya yanauzwa na lazima ufanye kazi ndipo upate hela ya kukuwezesha kunywa maji. Vivyo hivyo kula chakula, kuna gharama zake ambapo usipokuwa na fedha hauwezi kula. Hata vijijini unapata chakula baada ya kuwa umehangaika mashambani na kupata mazao ambayo ndiyo unayoyatumia kama chakula.

Katika burudani, kutazama mpira kwa mfano, kuna gharama zake, ambapo mtu hulipa kiingilio kwa ajili ya kwenda kuangalia mchezo wa mpira wa miguu. Hata katika uwanja wa mpira wa miguu hasa katika ligi kuu, kuna viingilio, kuonesha kwamba huwezi kufurahia kuangalia mchezo wa mpira wa miguu bila kulipia gharama, na ukiingia kule ndani uwanjani pia, kuna viwango vya mahali pa kukaa kwa ajili ya kuitazama hiyo mechi ambapo kama ulilipa pesa nyingi utapata kukaa sehemu nzuri zaidi na kinyume chake, ina maana kwamba uzuri wa sehemu na utamu wa kuangalia unapokuwa mzuri zaidi, ndipo na gharama ya kuangalia inapozidi kuwa kubwa sana.

Pia suala la kupata mtu wa kuishi naye, hapa tuongelee suala la kupata mke kwa mfano, ni gharama kubwa sana. Wanaume wengi watakumbuka jinsi ilivyokuwa taabu kwao kuwapata wenzi wao, hasa wakati wanachumbia. Kuna wengine walikuwa wanatukanwa hadi wanalia na kushindwa kula. Wanawake waliokuwa wanawataka walikuwa wakali sana na wanaowakatisha tamaa. Lakini kwa uwezo wa Mungu wanaume hawa wakiisha kutumia nguvu nyingi sana wanawapata wapenzi wao hawa na kuwa na mahusiano.

Lakini bado kuna gharama za uchumba. Ambapo wachumba wanalazimika kujichunga na kuhakikisha wanaondoa mapungufu yao kitabia, ili tabia zao zisiathiri mahusiano yao au hata kuyavunja. Baada ya uchumba ni ndoa. Upande wa mwanaume hutoa mahari, hugharimika kununua shela na kumpamba bi harusi, ndoa nyingi hutumia mamilioni ya fedha kufanyika. Na kwa maisha ya mkristo wa kweli haiwezekani kuoa bila kufunga ndoa, hali hii huleta gharama kubwa sana lakini zisizoepukika.

Baada ya ndoa gharama za maisha huanza, mwanamke atatakiwa kula, kuvaa na kunywa, kutibiwa akiugua na kutunzwa katika kila hali na mahitaji aliyonayo. Hapa naongea kwa mtazamo wa kibiblia ambapo mwanaume ndiye baba wa familia na kichwa cha nyumba.

Mwanaume ndiye anayetakiwa kuhakikisha kuwa mke yupo salama, anapata mahitaji yote. Na ndugu wa mke nao wanakuwa karibu kuhakikisha kuwa mtoto wao anatunzwa vizuri kule alikoolewa. Basi kuna wakati mwingine kana kwamba mzigo wa mwanamke pekee hautoshi, mashemeji nao huenda kwa zamu au kwa pamoja kuishi kwa 'shemegi’ yao.

Unaweza kufikiri kwanini mtu akimfumania mkewe ‘akichepuka’ anaweza kuua mtu? Ni kwa sababu ya gharama hizi tulizoziona hapo juu. Mwanamke avishwe apendeze, alishwe, atibiwe, na akishapendeza na kuwa na mvuto, ndipo mwanaume mwingine anakuja na kumuiba. Yaani akiwa mahututi hospitali, ni wa mumewe, akipona na kunawiri, anakuwa wa wote; inachukiza sana; haifai na usingependa kuona inatokea kwako, kwa hivyo usiifanye kwa mwingine. Kumbuka kuwa jambo lile usilopenda kufanyiwa, usimfanyie mwenzako.

Hizo hapo juu tulizoziona ni gharama za mke. Kwa hiyo tumeona kuwa huduma ya kuwa na mke ni ya gharama kubwa sana. Kwa sababu thamani ya huduma hiyo ni kubwa sana, ndivyo na gharama yake inavyokuwa kubwa. Njia yoyote ya mkato ya kuipata huduma hiyo, yaweza kusababisha mauti. Hilo halina ubishi, kwani mara ya mwisho nilisikia huko nyanda za juu kusini mchungaji alikutwa anazini na mke wa mtu akauawa.

Mwingine anawaza na kusema ‘mbona mwalimu unaongelea wanaume kutunza wanawake tu, wakati siku hizi kuna wanawake wanawagharimia waume zao,’ ni sawa, hiyo nayo ipo. Na inapokuwepo, tunaihesabu nayo kama gharama ambayo huyu mwanamke anaitoa kumgharimia mumewe, na asingependa kusalitiwa, ndiyo maana kuna wanawake huwa wanajiua pale wanaposalitiwa.

Kwa mifano hiyo na mengine tutakayoendelea kuiangalia tunaona kuwa kila huduma yenye kuleta tija au burudani kwa mwili au kwa mwanadamu inalipiwa na kadiri huduma hiyo inavyozidi kuwa nzuri na kubwa sana ndipo gharama yake inavyokuwa kubwa pia.

Gharama ya nafsi
Nafsi ya mwanadamu, ambaye ni mwanadamu mwenyewe ni ya thamani kubwa sana. Thamani ya nafsi ya mwanadamu hailinganishwi na kitu chochote kile, dhahabu hata ikijazwa duniani kote na kuongezewa maradufu haiwezi kufikia thamani ya nafsi ya mtu.

Kwa kuona thamani ya nafsi ya mwanadamu Mungu baba aliamua kumtoa Yesu Kristo afe msalabani ili kuikomboa nafsi ya mwanadamu na dhambi. Yohana 3:16.

Zinaa inagharimu nafsi
Licha ya kuwa nafsi ina thamani kubwa sana kiasi cha kumfanya Mungu atumie kila mbinu kuikomboa nafsi yako na hata kwa kumtoa mwanae afe msalabani, bado zinaa inaweza kubatilisha kazi kubwa iliyofanywa na Mungu ya kumtoa mwanawe pale msalabani kwani zinaa ina gharama kubwa sana ambayo ni nafsi yako. Yaani kwa maneno mengine ni kwamba huduma ya zinaa, kama ingekuwa inauzwa dukani, mtu angekuwa anatoa nafsi yake ili apatiwe huduma hiyo. Na katika ulimwengu wa roho ndivyo ilivyo, kwamba huduma hii haitolewi bure, na bei yake ni nafsi ya mwanadamu anayepatiwa huduma hiyo, hivyo kila ufanyapo zinaa unalipa, na malipo yake ni kuitoa nafsi yako na haiwi yako tena, unakuwa umeipeleka kwa yule mtoa huduma.
Tazama biblia inavyosema kuhusu jambo hili la zinaa kuwa na gharama ya nafsi

Mithali 6:32Mtu aziniye na mwanamke hana akili kabisa; Afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake.

KWANINI WATU WANAZINI/WANAKUWA WAZINIFU?

Usikose kufuatilia sehemu ijayo ya somo hili, ambapo tutaona sababu zinazowafanya watu kuwa wazinifu.

No comments:

Post a Comment