Friday, November 25, 2016

KUGEUKIA UKUTANI SEHEMU YA KWANZA

Mwandishi: Anderson Leng'oko

UTANGULIZI
Hili ni somo linalohusu maombi binafsi wakati unaokumbwa na tatizo kubwa ambalo linaweza hata kugharimu maisha yako. Ni wakati ambao unamuhitaji sana Mungu na hata huna muda wa kumtafuta mtu akusaidie kuomba. Unajikuta umebaki moyoni mwako wewe na Mungu wako hivyo unatakiwa kupeleka hoja na kumsihi Mungu akurehemu katika gumu upitialo.

MSITARI WA SOMO
Msitari wa somo hili unatoka katika kitabu cha Isaya 38:1-6
Siku hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona.
Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana,
akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana.
Ikawa, neno la Bwana likamjia Isaya, kusema,
Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako, asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano.
Nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu.

HABARI ZA HEZEKIA
Hezekia alikuwa mfalme wa Israeli, yeye huyu mfalme anatajwa kuwa alikuwa mwaminifu sana mbele za Bwana jambo ambalo lilimfanya apendwe na Mungu na katika wakati wa utawala wake Mungu aliwapiga wapinzani wa Israeli kwa mkono wake mwenyewe.
Hata hivyo ilifikia kipindi kama tulivyoona katika maandiko tunayosimamia katika somo hili kwamba Hezekia aliugua. Ugonjwa huu ulimfanya Mungu amtume nabii Isaya aende akamwambie Hezekia kwamba atengeneze mambo ya nyumba yake kwa maana ni ugonjwa ambao Hezekia asingepona.

Katika hali ya kawaida, Hezekia angekuwa ni mtu wa kawaida angeheshimu sauti ya nabii na kuandaa mambo ya nyumba yake. Lakini badala yake tunaona Hezekia akijigeuza, na kuelekeza uso wake ukutani, akimwomba Bwana.

Kwa kuwa Mungu ni mwaminifu na wa haki, anamsikia Hezekia na kumpa haja za moyo wake kama tulivyoona hapo juu ambapo anamuongezea miaka kumi na tano ya kuishi.

MAMBO YA KUJIFUNZA KUTOKA KWA HEZEKIA

HEZEKIA ALIKUWA NA MAHUSIANO BINAFSI NA MUNGU
Watu wengi huwa wanadhani Mungu anahusiana na watu kwa makundi. Mungu hahusiani na kanisa kama kundi bali Mungu anafanya mahusiano binafsi na mtu.
Ezekiel 22:30
Nami nikatafuta mtu miongoni mwao, atakayelitengeneza boma, na kusimama mbele zangu mahali palipobomoka, kwa ajili ya nchi, nisije nikaiharibu, lakini sikuona mtu.

Mungu kabla hajawa na mahusiano na kanisa zima, anatafuta kuwa na mahusiano na mtu mmoja mmoja kwanza. Hawezi Mungu kukaa na kanisa kama hana mahusiano na mtu mmojammoja kwenye hilo kanisa.
Ndiyo maana hata kwenye kuokoka wanasema unampokea Yesu Kristo kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako; wala siyo kumpokea Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wa kanisa lako. Tena wazungu wana msemo mzuri sana wanaposema “You receive Jesus as your personal saviour’’. Hili neno ‘personal savior’ lina maana ya mkombozi wako binafsi. Kwa hiyo Yesu anakuwa mkombozi wako binafsi na siyo wa kanisa, yaani Yesu anaanza kukuhudumia wewe kwanza halafu ndipo anahudumia kanisa kupitia wewe.

Faida za kuwa na mahusiano binafsi na Mungu

Mungu anakuwa anashughulika na shida zako moja kwa moja
Mungu anataka shida zako azishughulikie yeye ili apate sifa kupitia mafanikio yako. Mungu akishakuwa nyumbani kwako, moyoni mwako anakuwa ndiyo mtu wa kwanza kujua shida zako kabla hata rafiki yako hajajua. Hii inamfanya Mungu kushughulikia shida zako kwa wakati na kwa uhakika kabla hazijakuumiza.

Mungu anaweza kukutunzia siri zako
Mara nyingi sana watu wanakuwa na shida katika maisha yao lakini shida hizo wasingependa kuzikuta mtaani zimemwagwa na kila mtu anaziongelea. Mungu ndiye ajuaye sirini na yeye anaweza kukujibu na kukuhifadhi hadi ukapata haja au jawabu la tatizo lako bila mtu mwingine kujua.

Mungu ajuaye sirini ameahidi kuwajazi watu wamwombao
Mathayo 6:6
Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Yametokea matatizo mengi sana katika kanisa pale ambapo mpendwa unakuwa na tatizo lako na unaamua kuwashirikisha wapendwa wakuombee lakini matokeo yake wanaenda kukutangaza kwa watu na kukucheka mtaani. Hiyo isikusumbue, tengeneza mahusiano binafsi na Mungu ili uwe na uwezo wa kupambanua mambo ya kuwaambia watu na ya kubaki nayo mwenyewe. Na pia uhusiano mzuri na Mungu hukuepushia mambo ya fadhaa na matatizo kadha wa kadha ambayo watu huyapata kwa kutokuwa na uhusiano binafsi na Mungu.

Msaada wa karibu na wa haraka
Kuna wakati unahitaji msaada wa karibu na wa haraka sana kwa ajili ya shida zako. Kuna wakati mtu anahitaji maombi ya haraka, au wewe usiku wa manane umevamiwa na nguvu za giza, au mtoto wako mdogo sana amevamiwa na nguvu za giza. Unachotakiwa kufanya hapa ni kugeukia ukutani na kuomba kwa Mungu, na hii inakuwa ni rahisi sana kama utakuwa ni mtu wa kuimarisha mahusiano yako binafsi na Mungu.

Kuna watu hulazimika kuwatafuta wachungaji usiku wa manane kwa shida ambazo kimsingi kama wangetulia wenyewe na Mungu zingeweza kutatuka tu. Lakini zinawasumbua na kuwapotezea muda mwingi sana kwa kuchelewa kutafuta watu wa kuwaombea.

Watu kama hawa kwa kuchelewesha tatizo au kwa kushindwa kupata watu wanaofaa hujikuta wakisumbuliwa hadi wanafikia kiwango cha kugeukia miungu mingine iwatatulie shida zao wakidhani kuwa Mungu ameshindwa au hawezi.

Hii ni kutokana na ukweli kuwa kwa kukosa mahusiano binafsi na Mungu wanakuwa hawana mizizi thabiti ya imani na hivyo kuyumbishwa na matatizo.

Usikose kufuatilia sehemu ya pili ya somo hili, waalike na wengine pia washiriki nasi baraka hizi.


No comments:

Post a Comment