Monday, May 19, 2014

UTAFUTE UFALME WA MUNGU KWANZA

OUR DAILY MANA


UTAFUTE UFALME WA MUNGU KWANZA

Karibu tena mpendwa katika Bwana katika darasa letu la kujifunza maandiko katika mfululizo huu. Somo liliopita tuliangalia juu ya kuhakikisha kuwa jina lako linajulikana mbinguni; na tukaona kuwa unaweza kuwa ni mtumishi hapa duniani lakini jina lako likawa halijulikani kwa Mungu. Leo tunataka tuangalie walau kwa ufupi juu ya suala la kuutafuta ufalme wa Mungu kwanza, kabla ya mambo mengine.

Watu wengi hasa kwenye ulimwengu wa leo wameweka kipaumbele kwenye kutafuta kile wanachokiita ‘MAISHA.’ Utawasikia watu wengi wakisema kuwa ‘ninatafuta maisha.’ Katika suala hili kunahusisha mambo mengi; wako wanaohangaika kutafuta elimu; wengine wanatafuta ajira; wengine wanatafuta wapenzi; wengine wanatafuta mambo ya kibishara; n.k. Katika kutafuta kwao watu wengi wamejikuta wakikosa muda kabisa wa kuutafuta uso wa Mungu. Na ukipata nafasi ya kuwauliza, jibu lao ni kuwa muda hautoshi.

Nimejaribu kulichunguza jambo hili kwa umakini mkubwa nikagundua kuwa, shetani ametengeneza mkakati mkubwa sana wa kuwatenga watu na Mungu wao kwa kutumia mahitaji ya kila siku ya maisha. Katika kuchunguza maandiko nikagundua kuwa Biblia haijanyamaza kuhusu suala hili.
Mathayo 6: 25, 31-33 inasema hivi:
Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? … Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.
Haya maneno yanatuambia kuwa Mungu anajua kila tunachokihitaji, na kwamba haitupasi kusumbuka kuyatafuta hayo ila tuutafute kwanza ufalme wake na haki yake na hayo mengine tutazidishiwa. Iko siri ya ajabu sana kwenye maneno haya ambayo imetupasa kuifua kabla hatujasonga mbele.
Mtume Paulo anatuambia jambo la ajabu sana kwenye Wafilipi 4:19. Anasema; “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.”
Huu msitari unaonesha kuwa uko utajiri wa kutosha ndani ya kristo na Mungu yuko tayari kuwajaza wale wamtafutao kila wanachokihitaji. Ni ajabu sana neon hili. Je, inamaana hatupaswi kufanywa kazi? Je, ni nini maana ya kuutafuta ufalme wa Mungu na haki yake?
Daudi anaanza kutupa majibu ya maswali haya katika Zaburi 27:8. Inasema hivi: “Uliposema, Nitafuteni uso wangu, Moyo wangu umekuambia, Bwana, uso wako nitautafuta.” Daudi anatuonesha kuwa Mungu alitoa tangazo kuwa watu wamtafute uso wake, nay eye Daudi akajiweka tayari ili autafute uso wa bwana. Kwa nini ilikuwa ni muhimu autafute uso wa Bwana?
Kitabu cha 2 Nyakati 26: 5 inasema: “Akajitia nia amtafute Mungu katika siku za Zekaria, aliyekuwa na fahamu katika maono ya Mungu; na muda alipomtafuta Bwana, Mungu alimfanikisha.
Iko siri ya ajabu sana kwenye huu msitari. Biblia inasema huyu ndugu alijitia nia (hebu sema, nia) ili amtafute Mungu. Na alipoanza kumtafuta Bwana, Mungu akaanza kumfanikisha kwenye mambo aliyokuwa anayafanya. Huyu ndugu Uzia alikuwa mfalme, na Biblia inatuambia alianza kutawala akiwa na umri wa miaka 16. Hebu fikiria leo, kijana wa miaka 16 apewe kuingoza nchi atafanyaje? Lakini Uzia yeye aliamua kumtafuta Bwana kwanza. Kwa nini? Kwa sababu alijua kuwa hakuna namna nyingine yoyote ambayo angeitumia kuendesha nchi ile akafanikiwa isipokuwa amemtafuta Mungu kwanza.
Leo hii watu wengi wanatumia muda mwingi sana kutafuta majibu ya matatizo yao ya kimaisha kwa sababu wamesahau mahali ilipo chemchemi ya mafanikio yao. Mungu anashangaa sana jinsi watu wake walivyopotea kwa kuamua kujitafutia wenyewe majawabu ya maisha yao huku wakiwa wamemsahau yeye. Katia Yeremia 2:13 anasema:
Kwa maana watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji.
Mungu anasema watu wake wamejichimbia mabirika yavujayao, yasiyoweza kuweka maji. Maana yake licha ya kuwa wanahangaika sana kutafuta maisha, bado hawafanikiwi kwa sababu wamemweka mbali yeye aliye chemchemi ya mafanikio yao. Ndiyo maana licha ya watu kuamua kufanya kazi mpaka siku za ibada na kumsahau Mungu, bado mambo yao hayaendi vizuri.
Iko faida ya kuutafuta uso wa Mungu kwa sababu, pindi unapomtafuta Mungu yeye anakufanya kufanikiwa. Marko 10: 28-30 inasema hivi:
Petro akaanza kumwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe. Yesu akasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.
Ukiamua kuutafuta ufalme wa Mungu na haki yake, Mungu anakufanikisha mara mia na kukupa uzima wa milele kwenye ulimwengu ujao. Biblia inasema hayo mengine ni ziada tunayozidishiwa pale tunapoweka suala la kumtafuta Mungu namba moja.
CHAGUA KUMTAFUTA MUNGU KWANZA
YESU YU KARIBU KUJA
 

No comments:

Post a Comment