Saturday, May 17, 2014

JE, JINA LAKO LINAJULIKANA MBINGUNI?

OUR DAILY MANA


JE, JINA LAKO LINAJULIKANA MBINGUNI?

Karibu tena ndugu yangu katika Kristo katika sehemu yetu ya Kujifunza maandiko ili tupate kuukulia wokovu. Leo nina mada iliyo katika mfumo wa swali. Swali hili nahisi ni muhimu mno kwa mtu yeyote aliye kwenye safari ya kuelekea mbinguni akajiuliza mapema.

Katika utaratibu wa duniani, mtu anaweza akaenda sehemu hata kama hafahamiki lakini akajitambulisha na kuelezea alikotoka na kilichomleta, kisha akapokelewa kama vile alikuwa anafahamika tangu zamani. Huu ni utaratibu mzuri kwa sababu unakupa uhakika wa kupokelewa sehemu yoyote unayooenda hata kama wewe mwenyewe unajua kuwa unakokwenda hawakufahamu. Kwa bahati mbaya sana utaratibu wa mbinguni ni tofauti kabisa na huu tunaotumia hapa duniani. Utaratibu wa mbinguni unataka mtu awe anafahamika mbinguni tangu akiwa duniani, ili siku akienda wasipoteze muda kumjua yeye ni nani?

Kilichonisukuma mpaka kuleta ujumbe huu kwako kinatoka pale Kutoka 33:17.unasema
“Bwana akamwambia Musa, Nitafanya na neno hili ulilolinena, kwa maana umepata neema mbele zangu, nami nakujua jina lako.”

Jambo la ajabu tunalojifunza kutoka kwenye msitari huu ni kuwa Mungu aliamua kufanya kile ambacho Musa alikuwa ameomba kwa sababu Mungu alimjua jina lake. Kitu cha kujiuliza hapa ni kuwa kulikuwa na umuhimu gani wa Mungu kumwambia Musa kuwa nakujua jina lako?

Ni ajabu sana kugundua kuwa licha ya kuwa Mungu alitembea na Musa tangu kabla ya kutoka Misri lakini anakuja kumtangazia kuwa anamjua jina lake huku mwishoni kabisa mwa kitabu cha Kutoka. Ni nini Mungu alitaka tuone hapa?

Katika Mathayo 7:21 Yesu anasema “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.” Kwa lugha nyingine Yesu alikuwa anasema kuwa si kila mtu anayelitaja jina Bwana anajulikana mbinguni,bali ni yule ambaye anayafanya mapenzi ya Baba yetu aliye mbinguni. Maana yake unaweza kuwa unafikiri unamtumikia Mungu kumbe unayatumikia mapenzi yako mwenyewe au mapenzi ya wanadamu.
Katika Luka 13: 25-27 Yesu aliwaambia watu akasema
Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako; ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu. Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu.
Hii inatufunulia kujua kuwa kuna kitu zaidi ya kutumika ambacho ndicho kinachompa mtu nafasi kwenye ufalme wa Mungu. Kitu hicho ni JINA LAKO KUJULIKANA MBINGUNI. Ndiyo maana Yesu akasema “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” (Mathayo 7: 22-23)
Haya maneno yanatisha sana, hawa ni watu waliokuwa wakimtumikia Yesu duniani lakini siku ya mwisho anawaambia dhahiri kuwa hawajulikani mbinguni. Kwa nini? Matendo 13: 36 inatupa jibu. Inasema: “Kwa maana Daudi, akiisha kulitumikia shauri la Mungu katika kizazi chake, alilala…
Kumbe ni kulitumikia shauri la Mungu ndiko kunakufanya ujulikane mbinguni. Unaweza kuwa unatumika kumbe unatumikia shauri la mchungaji wako, au shauri la wazazi wako, au shauri lako mwenyewe. Jiulize kwanza, utumishi unaofanya unafanya ili kumridhisha nani? Ukiona kuwa unafanya kwa sababu ya mtu Fulani ujue jina lako halijulikani mbinguni. Lakini pia kuyafanya mapenzi ya Mungu kunaambatana na kuacha dhambi na kuamua kuwa mwaminifu kwa Bwana. Ukikosa uaminifu kwa bwana ujue wazi kuwa jina lako halijulikani mbinguni. Unaweza kusema kuwa unayafanya mapenzi ya Mungu eti kisa unaona Mungu akionekana katika utumishi wako. Ooooh my friend its more than that. Mungu anaweza kushuka kwenye huduma lakini asishuke kwako. Huduma inaweza kufanikiwa kupitia wewe lakini wewe ukawa huna nafasi mbinguni. Ndiyo maana Paulo akasema “bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa. 1 Kor 9:27
Kumbe unaweza kuwahubiri wengine halafu wewe ukawa mtu wa kukataliwa, yaani ukawa hujulikani mbinguni. Oooh nakupa shauri leo uhakikishe jina lako limeandikwa mbinguni.
HAKIKISHA UNAJULIKANA MBINGUNI
YESU ANAKUJA UPESI NA UJIRA MKONONI
 

No comments:

Post a Comment