Friday, September 22, 2017

UNAFANYA ZIADA GANI? (SEHEMU YA NNE)

  

Mwandishi: Anderson Leng'oko

ZIADA YA MSAMARIA MWEMA

Utangulizi
Kwa neema ya Mungu bado tuna vitu tunavijadili kuhusu kufanya ziada, na leo tunakijadili kisa maarufu cha Msamaria mwema. Karibu ujifunze nasi, na kama hujasoma sehemu zilizotangulia na ungependa kupata mtiririko mzuri bonyeza hapa.

Luka 10:30-35
Mtu mmoja alishuka toka Yerusalemu kwenda Yeriko, akaangukia kati ya wanyang'anyi; wakamvua nguo, wakamtia jeraha, wakaenda zao, wakimwacha karibu ya kufa.
Kwa nasibu kuhani mmoja alishuka kwa njia ile; na alipomwona alipita kando.
Na Mlawi vivyo hivyo, alipofika pale akamwona, akapita kando.
Lakini, Msamaria mmoja katika kusafiri kwake alifika hapo alipo; na alipomwona alimhurumia,
akakaribia, akamfunga jeraha zake, akizitia mafuta na divai; akampandisha juu ya mnyama wake, akampeleka mpaka nyumba ya wageni, akamtunza.
Hata siku ya pili akatoa dinari mbili, akampa mwenye nyumba ya wageni, akisema, Mtunze huyu, na cho chote utakachogharimiwa zaidi, mimi nitakaporudi nitakulipa.

Hii ni hadithi ambayo husomwa na inajulikana sana, inaitwa hadithi ya Msamaria mwema. Katika historia, watu wa Samaria(wasamaria) na watu wa Yuda(wayahudi), walikuwa hawapendani kabisa na chuki yao ilifikia hadi hatua ya kutokupeana hata maji ya kunywa.

Yohana 4:7-9
Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe.
Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula.
Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.)


Umeona? Kama hizi jamii mbili zilikuwa hata kupeana maji hazipeani, maana yake ni kwamba kulikuwa hakuna namna Msamaria angeweza kumkuta myahudi amepigwa njiani akamsaidia; sanasana angeshangilia kama ilivyo kawaida ya wengi wetu kushangilia pale adui anapopatwa na jambo baya.

Huyu Msamaria alikuwa haishi kwa kufuata historia wala mkumbo. Yeye alijua kuwa yule mtu aliyepigwa licha ya kuwa alitoka kwenye jamii iliyokuwa ni ya adui lakini alikuwa ni mwanadamu kama yeye na alihitaji msaada.

Yeye hakujali ule uadui. Katika hali ya kawaida isingekuwa rahisi kupuuzia uadui uliokuwapo kati ya Samaria na Uyahudi. Lakini Msamaria huyu aliona kuwa hakikuwa kikwazo cha yeye kumsaidia huyu mtu.

Mambo kadha wa kadha alifanya Msamaria mwema kwa mtu huyu, Myahudi:
-          Hakujali kupoteza muda wake, kwa kawaida mtu unaposafiri unakuwa na bajeti umeipanga ya kutumia muda. Kama ulikuwa umepanga kusafiri kwa siku tatu, utajitahidi usafiri kwa siku angalau tatu kamili au basi zipungue ziwe mbili, ili uweze kukutana na familia yako mapema inavyowezekana. Lakini msamaria huyu hakujali kama alikuwa anapoteza muda wake kwa kuchelewa kufika kule anakokwenda kwa sababu ya kumsaidia mtu ambaye kiasilia alikuwa wa jamii ya adui zake.

-          Hakuogopa kuvamiwa na majambazi. Wengi katika haya maisha tunajua kuwa ukipita katika njia inayotisha unafanya haraka sana kupita hayo maeneo ili usije ukavamiwa. Ile njia ilikuwa mbaya sana; ukiwaangalia wataalamu wanasema ilikuwa ni njia yenye milimamilima na ya kutisha, ilikuwa ni njia ambayo haikuwa salama hata kidogo, kwa hivyo kila mtu aliyepitia hii njia alikuwa katika mwendo wa kukimbia ili angalau apite haraka bila kuvuta umakini wa majambazi. Lakini msamaria mwema alipofika hapa akamkuta mtu amepigwa aliondoa hofu na kuamua kufanya tendo la huruma bila kujali kuwa na yeye alikuwa anahatarisha usalama wake. Jambo hili lingekuwa rahisi kama mtu huyu angekuwa anamsaidia ndugu yake labda; lakini ikumbukwe kuwa msamaria huyu hapa alikuwa anapoteza muda wake kama tulivyoona hapo juu na pia alikuwa anaweka rehani usalama wake na hata uhai wake kwa kumsaidia adui yake.

-          Msamaria mwema huyu pia alitumia vitu vyake vya safari. Biblia inatuambia kuwa msamaria mwema alizitibu zile jeraha kwa divai na mafuta. Vitu hivi vilikuwa ni vitu ambavyo msamaria mwema alikuwa amejibebea kwa ajili ya safari na angependa visiishe. Lakini kwa ukarimu wake alionao, alitumia vitu hivi kumsafishia myahudi vidonda. Hapa msamaria alikuwa anatoa vyote alivyo navyo kumsaidia adui. Ni jambo adimu sana katika maisha ya sasa.

-         Msamaria mwema pia alitoa fedha zake. Alikwenda na mgonjwa huyu hadi mjini, akampangishia hoteli kwa gharama yake na alimkabidhi huyu mtu kwa muhudumu, akampa na yule mhudumu kiasi cha pesa, ambapo kama kingepungua aliahidi kurudi na kuongezea. Hapa wapendwa najaribu kuona ni kwa jinsi gani msamaria mwema huyu alijihakikishia usalama wa safari yake. Huwezi ukasafiri kwa uoga katika safari kama hiyo kwa sababu kwa hakika Mungu hawezi kukuacha ukaumizwa safarini ukiwa umetenda matendo yaliyougusa moyo wa Mungu kwa kiwango kikubwa namna hiyo.

-         Hapo kumbuka kuwa yule myahudi aliyesaidiwa alikuwa ana moyo wa shukrani kwa msamaria huyu. Lazima uwe na uhakika kuwa myahudi yule atamuombea yule msamaria kwa Mungu wake na kumbariki usiku na mchana; hii itaongeza kiwango cha mafanikio katika safari ya msamaria huyu. Na msamaria huyu ndani yake kana kwamba alikuwa hajatosheka na aliyoyatenda, alikuwa bado anataka kurudi ili kumalizia gharama za yule aliyemhudumia.

-         Msamaria mwema pia alikuwa mfuatiliaji. Watu wengi wanafanya huduma ya Mungu siku hizi lakini wanasahau kipengele hiki cha ufuatiliaji. Ukisoma hapo utaona kuwa msamaria mwema aliahidi kurudi na kujua kuwa kiasi gani kimeongezeka katika kumtunza na kumtibu yule myahudi. Siku moja nilipokuwa nahudumu kupitia door to door, (kushuhudia injili nyumba kwa nyumba - mitaani), nilimshuhudia dada mmoja na baada ya kama wiki moja hivi tulirudi kwake tena tukiwa tunamuangalia anaendeleaje. Ni kweli kuwa mume wa yule dada tulikuwa mwanzoni hatukumkuta, bali tulimkuta mkewe, mkewe alikuja kumwambia habari zetu, lakini yeye anasema alidhani sisi ni kama wainjilisti wengine tu aliowazoea ambao huja mara moja na wakiondoka hawarudi tena. Lakini sisi alitushangaa sana na akamshukuru Mungu kwa ajili yetu kwa vile tulivyorudi tena kuona anaendeleaje, tulikuwa tumeonesha upendo mkubwa sana kwake kwa kufanya vile.

Ufuatiliaji ni jambo la msingi sana katika huduma, ni vyema kufuatilia watu tunaowaleta kwa Kristo ili tuhakikishe kwamba mbegu tuliyoipanda inamea. Hayo tuliyoyaona hapo juu ni mambo ya ziada ambayo kama Msamaria mwema akiulizwa na Mungu “Ulifanya ziada gani?” basi huyu msamaria mwema atayataja mambo hayo hapo juu. Je na wewe ukiulizwa leo, Unafanya ziada gani, utajibu kitu gani? Tafakari… Unafanya ziada gani???


No comments:

Post a Comment