Monday, July 10, 2017

UNAFANYA ZIADA GANI? (SEHEMU YA PILI)

Mwandishi: Anderson Leng'oko

Utangulizi
Tuliona katika sehemu ya kwanza kuwa kuna umuhimu wa kufanya ziada; leo katika kuendelea na somo letu, tutaangalia baadhi ya mambo ambayo tutafaidiwa sana tukiyafanya kwa umuhimu na bidii kubwa. Vipo vitu katika maisha ni vya kuvipa kipaumbele na kuvifanya kwa bidii, kwani matokeo yake huzidi kuwa bora tunavyozidi kuvifanya kwa wingi. Kama hukusoma sehemu ya kwanza basi bonyeza hapa ili upate mtiririko mzuri wa somo letu. Mungu akubariki unapoendelea kujifunza nasi.





KUFANYA ZIADA
Mambo yafuatayo ni baadhi tu ya mambo ambayo unatakiwa kuyapa kipaumbele katika kufanya ziada


-          Kuomba na kusoma neno la Mungu
Mambo haya ukiyafanya zaidi ya mafarisayo na ukayafanya kwa kumaanisha; au ukiyazidisha kuyafanya katika maisha yako, usiombe kwa unafiki, au ukazidisha muda wa kuomba kwa kumaanisha, basi wewe unaurithi ufalme wa Mungu lakini pia utaweza kuepuka mitego iliyowanasa mafarisayo. Pia katika kusoma neno la Mungu, watakiwa kufanya ziada, yaani ‘zaidi ya kawaida’, au basi ukiweza, zaidi ya wengine wote. Ndipo uwepo wa Mungu utakapojaa ndani yako na hutafukuzana na dhambi bali dhambi itakukimbia.

-          Kutenda mema
Hapa tena ndipo Yesu amesisitiza sana. Yaani kwamba utende mema zaidi ya wamataifa watendavyo. Kuwapenda adui na kutokuwachukia watu kama tulivyoona. Lakini hapa ikumbukwe kuwa huwezi kuyakamilisha haya kwa ukamilifu kama hautakuwa na ziada katika kuomba, kufunga na kusoma neno la Mungu. Mambo haya yanategemeana. Kama unataka kuwazidi mataifa katika jambo lolote lazima kwanza uanze kuwazidi katika kuomba, kufunga, na kusoma neno la Mungu.

-          Kumtumikia Mungu
Unapomtumikia Mungu usimtumikie kama mafarisayo, usitafute kujifaidisha wewe mwenyewe bali utafute kuueneza ufalme wa Mungu pasipo na hila moyoni mwako. Angalia utumishi wa mafarisayo anaouongelea Yesu;
Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache.
Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia.
Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi.
Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi.
Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.
Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi. (Mathayo 23:23-28)

Hapo tunajifunza kuwa mafarisayo wanafuata sheria sawasawa katika utumishi wao, na dalili za nje za kuonekana; lakini wameachana na utakatifu. Yesu anawatajia mafarisayo vitu muhimu vya kuwa navyo ambavyo hata wewe mtumishi wa Mungu unatakiwa kuwa navyo ili kuifanya haki yako izidi kuwa zaidi ya ile ya mafarisayo: adili, rehema na imani.

Mafarisayo wanaonekana kwamba hawakuwa na utu wema wa ndani, hawakuwa na maadili wala hawakuutafuta utakatifu. Ndicho ambacho Yesu anatamani sisi wanafunzi wake tuwe nacho.

                    Yale mengine msiyaache
Licha ya kuwa Yesu anawahimiza mafarisayo kuzingatia adili, rehema na imani; anawasisitiza kuwa yale mengine wasiyaache. Hii ina maana kuwa vitu vyote vina umuhimu wa kipekee katika kumtumikia Mungu. Mengine anayoyazungumzia Yesu ni pamoja na zaka na kanuni zingine za imani kwa mujibu wa kanisa. Kwa sasa watumishi wa Mungu wengi wanakutana na changamoto nyingi za kimaisha hadi wanakuwa wanashindwa kuwa waaminifu kwenye suala la matoleo.
Hilo siyo jambo jema na kamwe Mungu hafurahishwi nalo, Mungu anataka uwe msafi moyoni lakini kanisani pia umtolee. Wengine wanakuwa wanafanya yote hayo lakini hawataki kuwashuhudia wengine kwa habari ya Kristo wala hawataki wengine wajue kuhusu imani yao, ni sharti la Ukristo kuungama mbele ya mashahidi wengi na kumtangaza Kristo katika semina na uinjilishaji. Kwa hiyo wewe usiishie tu kuwa mkristo wa kuokoka kwa siri, kama ambavyo wengi wanasema ‘wewe ukiokoka unajua wewe na moyo wako usimwambie mwingine,’ hapana, usiwashe taa ukaiweka chini ya uvungu; inuka uangaze…
Luka 8:16
Hakuna mtu ambaye akiisha washa taa huifunika kwa chombo, au kuiweka mvunguni, bali huiweka juu ya kiango, ili waingiao wapate kuona nuru yake.
Isaya 60:1
Ondoka, uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, Na utukufu wa Bwana umekuzukia.

ZIADA HUKUPA UWEZO ZAIDI YA WENZIO
 Waebrania 1:9 Umependa haki, umechukia maasi; Kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta, Mafuta ya shangwe kupita wenzio.

Mungu anakuahidi furaha na shangwe kupita wenzio kama utachukia maasi na kupenda haki. Hapa inatuonesha kuwa hao wenzio siyo lazima wawe wapagani, ila inawezekana nao pia wanapenda haki, ila ukiwazidi katika kupenda haki, na furaha yako itakuwa kubwa zaidi yao.

Unaweza kuzidi katika mambo kadha wa kadha, na katika kila jambo, ukizidi, na furaha yako au matokeo yako yatawazidi wengine. Ni kama darasani, kama utakuwa makini zaidi darasani na kufanya bidii zaidi ya wenzako na kuelewa zaidi yao, matokeo yako yatakuwa bora zaidi. Na pia katika Mungu kama wewe utakuwa mwombaji zaidi na mfungaji zaidi na mwenye kusaidia watu zaidi, baraka zako zitawazidi wote unaowazidi kuomba na kufunga.
Fanya ziada ya kazi upate ziada ya matokeo; Mungu yupo na wewe kukuzidishia wewe uliyezidi katika kumtafuta; Mungu yupo kukuzidishia nguvu zake wewe uliyezidi katika kuomba na kufunga, Mungu yupo kukuzidishia uwepo wake wewe unayemtafuta usiku na mchana. Mungu yupo kukupa hitaji lako wewe uliyezidi katika kumtegemea na kumuamini yeye. Mungu yupo katika kukuokoa na kukulinda wewe uliyezidi katika kuwasaidia wengine. Mungu yupo katika kukubariki wewe uliyezidi katika kumtolea yeye na atahakikisha unazidi katika kipato hadi watu washangae; fanya ziada ili upate ziada, apandaye haba atavuna haba. Unafanya ziada gani?

Usikose sehemu inayofuata ya somo hili, unaweza kulisambaza pia ili wengine nao wazidi kubarikiwa na ujumbe huu. Ubarikiwe sana.




No comments:

Post a Comment