Thursday, June 15, 2017

UNAFANYA ZIADA GANI? (SEHEMU YA KWANZA)


Mwandishi: Anderson Leng'oko

Utangulizi
Mafundisho ya Bwana Yesu ni ya ajabu sana, nayo yanaleta raha sana na kutufariji mara tuyasomapo. Kila nisomapo mafundisho ya Bwana Yesu huwa ninajazwa nguvu mpya na kuiona upya ile faida na furaha ya wokovu ulio ndani yangu. Yesu anatufundisha mambo mengi sana ya msingi na sisi watu wake tunatakiwa kuyajali mafundisho yake na kuweza kuyatumia kurutubisha roho zetu. Mafundisho ya Yesu yanatufaa kama ambavyo chakula kifaavyo kwa mwanadamu; kama ambavyo maji yafaavyo kwa wenye kiu na kama ambavyo pumzi ni muhimu kwa kiumbe hai.
TULIANGALIE SOMO HILI
Katika somo hili tumepewa kichwa cha habari kisemacho “Unafanya Ziada Gani?” maneno haya yametolewa katika moja ya mafundisho aliyoyatoa Yesu kwa watu waliokuwa wanamsikiliza kama ilivyokuwa kawaida yake; hebu tuiangalie mistari hiyo ili tuone Yesu anafundisha kitu gani-
Mathayo 5:38-48

Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili.

Akuombaye, mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo. Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.

Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?

Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.

Yesu alikuwa anawafundisha wanafunzi wake namna ya kuishi na watu na njia mpya ya utakatifu. Nasema hii ilikuwa ni njia mpya kwa sababu wale watu kabla ya hapo walikuwa wanaishi kwa kanuni ya jino kwa jino.

Kuna jambo la kupatikana na ziada
Katika mistari hiyo hapo juu Mungu anahimiza sana ziada. Anasema lazima matendo yetu kama Wakristo tuyafanye kwa uzuri uliozidi yale ya wa mataifa. Watu wengi wamejaribu kuyafumbia macho mafundisho haya. Lakini ni kweli kuwa mafundisho haya hayaepukiki.

Lakini nadhani kama kanisa lingeyaishi mafundisho haya, ugomvi mwingi sana ungekuwa unakwisha bila kuhusisha waamuzi. Yaani kama kila mtu angekuwa wa kwanza kumsalimia na kumsaidia adui yake kama maneno yanavyosema hapo juu, basi mapatano yangeenea kila mahali.

Ndicho ambacho Yesu alileta duniani; Yesu alileta amani na ndiyo maana anaitwa Mfalme wa Amani.
Yesu anatamani kwamba kama kuna mambo ya kufanya yenye wema; Wakristo ndio watu ambao wanatakiwa kuwa wamewazidi wanadamu wote kwa sababu wao wanafanya na ziada. Kama ni wema; wakristo wanatakiwa kuwa wanawazidi wote wanaofikiri kuwa wanafanya wema; kama ni huruma na upendo vilevile.

Wakristo katika kusamehe pia wanatakiwa kuwa wamezidi; na hapa Yesu anatoa mfano wa Mungu anapowaangazia jua wabaya na wema. Ni jambo la muhimu sana kujifunza kwa maana kwamba Mungu kama mjenzi na anayeitunza dunia asingependa watu wanaomchukia waendelee kuitumia dunia yake; lakini hajafanya hivyo; bali ameendelea kuwaangazia jua wote wakorofi na wema; na zaidi ya hayo anawanyeshea mvua wote bila kujali kuwa huyu ni mwema au ni mbaya.

Yesu ameyarudiarudia sana hayo mafundisho yake katika kusisitiza hoja yake. Watu ambao wanaweza kudhani kuwa Yesu alikuwa na maana nyingine katika mafundisho hayo wanahitaji pia kusoma mistari ya ziada ili waweze kujiridhisha kwamba Yesu alikuwa ana maana hiyo hiyo ya kufanya ziada. Yesu alitaka wakristo wawe ni watu waliozidi katika wema na wasiojihusisha kabisa katika ubaya.

Uitapo watu karamuni

Luka 14:12-14
Akamwambia na yule aliyemwalika, Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo.
Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu,nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.

Yesu anaendelea kusisitiza utofauti na uziada katika matendo yetu sisi wateule wake. Hapa anatuamuru tufanye ziada katika kuandaa karamu na kuwaalika watu. Anataka tuwe na mtazamo tofauti katika lengo la kuandaa karamu. Hii ni ziada ya wema anayotaka tuifanye; ya kuwaalika masikini, vilema na vipofu.

Ni ziada kwa misingi kwamba; Yesu anajua kwamba watu hualikana kwenye karamu kwa misingi ya kuweka akiba ili nao siku moja wafanyiwe hivyo; au huandaa karamu na kuwaalika rafiki zao ili kuwalipa mema ambayo walishawahi kufanyiwa hapo kabla, lakini Yesu anatufundisha kuwa licha ya kuwa kuwaalika rafiki zako karamuni au kuwaandalia karamu ni jambo jema; lakini la kuwasaidia na kuwaita wale ambao hawawezi kukusaidia ni vyema zaidi kwani wao hawawezi kukulipa. Kwa hiyo tukifanya hivyo; yaani kuwaalika masikini karamuni, tutakuwa tumetenda ziada, tukiwazidi watu wa kawaida ambao wao hualika rafiki zao tu karamuni.

Haki yenu isipozidi ya mafarisayo
Hili ni jambo jingine lililoonesha katika biblia kwamba Yesu anatafuta ziada ndani ya wateule wake…Angalia hapa anasisitiza hadi anaonekana kuwa radhi kuwakosesha wateule wake uzima wa milele kwa sababu tu ya kutokuwa na ziada katika wema na matendo matakatifu. Sikiliza, ni kweli kwamba hatuwezi kujitengenezea haki kwa matendo yetu lakini tunatakiwa kujivika utakatifu na kuwa matajiri katika kutenda mema. Hebu tuiangalie hii habari ya kuwazidi mafarisayo…

Mathayo 5:20 Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.

Lakini hapa tunaweza kujiuliza neno moja, kwani mafarisayo walikuwaje?
Mathayo 23:2-33
Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa;basi, yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi.
Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao.Tena matendo yao yote huyatenda ili kutazamwa na watu; kwa kuwa hupanua hirizi zao, huongeza matamvua yao;hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi,na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi.

Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu.Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni.Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu.
Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie.

Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnakula nyumba za wajane, na kwa unafiki mnasali sala ndefu; kwa hiyo mtapata hukumu iliyo kubwa zaidi. Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanum mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe.

Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga. Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo kubwa, ile dhahabu, au lile hekalu liitakasalo dhahabu? Tena, Mtu atakayeapa kwa madhabahu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa sadaka iliyo juu yake, amejifunga. Vipofu ninyi; maana ni ipi iliyo kubwa, ile sadaka, au ile madhabahu iitakasayo sadaka?

Basi yeye aapaye kwa madhabahu, huapa kwa hiyo, na kwa vitu vyote vilivyo juu yake.
Naye aapaye kwa hekalu, huapa kwa hilo, na kwa yeye akaaye ndani yake. Naye aapaye kwa mbingu, huapa kwa kiti cha enzi cha Mungu, na kwa yeye aketiye juu yake. Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache.

Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia.Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi. Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi.

Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.
Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.

Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnayajenga makaburi ya manabii, na kuyapamba maziara ya wenye haki, na kusema, Kama sisi tungalikuwako zamani za baba zetu, hatungalishirikiana nao katika damu ya manabii. Hivi mwajishuhudia wenyewe, ya kwamba ninyi ni wana wao waliowaua manabii. Kijazeni basi kipimo cha baba zenu. Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya jehanum?

Tunaweza kuorodhesha sifa chache za mafarisayo
-          Walikuwa hawatendi wanachokihubiri
-          Walikuwa wanafiki
-          Walikuwa watu wa kujionesha kuwa wamekubalika
-          Walikuwa wanawazuilia wengine kumjua Mungu
-          Walikuwa hawamuogopi Mungu ndani ya mioyo yao
-          Walikuwa hawana mahusiano binafsi na Mungu
-          Walikuwa hawana mahusiano mazuri na waumini wao.
-          Walikuwa siyo watu wa kutenda haki
-          Walikuwa watu wa kupindisha mafundisho ili kujitengenezea faida binafsi.

Kwa hiyo Yesu alitamani wanafunzi wake na kila aliyetamani kuurithi uzima wa milele kutenda zaidi ya mafarisayo ili astahili kuurithi uzima wa milele. Hii inaonesha kuwa mafarisayo walikuwa hawawezi kuurithi uzima wa milele. Mafarisayo walishika sheria zote za mafundisho ya kidini lakini walisahau kuutafuta utakatifu na kuyaishi yale waliyokuwa wakiyafundisha.

Hili jukumu la kufanya zaidi ya mafarisayo halikuishia tu kwa wanafunzi wa Yesu, bali linaendelea hadi leo; naomba hapa usiniulize kama mafarisayo bado tunao, maadamu tumeshaona hapo juu mapungufu yao basi ni kazi yako kuamua kama tunao au la; ila kama usipowaona basi wewe tafuta kufanya zaidi ya mafarisayo waliokuwa wakiishi wakati wa Yesu.


Usikose kuendelea kujifunza pamoja nasi somo hili zuri katika sehemu ijayo. Ubarikiwe sana.

1 comment: