Thursday, February 9, 2017

KUGEUKIA UKUTANI (SEHEMU YA TANO)

 Mwandishi: Anderson Leng'oko

Utangulizi
Mpendwa msomaji, upo wakati ambapo unabaki peke yako katika maisha yako ya huduma, kazi au familia. Hapa unatakiwa kupata msaada toka kwa Mungu wako. Ndipo ambapo unatakiwa kugeukia ukutani umlilie Mungu ili akusaidie. Katika sehemu hii ya tano ya somo hili, tunaendelea kuangalia watumishi mbalimbali ambao walimgeukia Mungu naye akawasaidia.Kwa kusoma sehemu nyingine zilizotangulia bonyeza hapa.

Ipo hadithi ya mfalme Daudi, ambapo mfalme Daudi alimpenda mke wa mtumishi wake, mke wa Uria, akalala naye akampa mimba. Akafanya mpango wa kumuua Uria ili amuoe yule mwanamke, kweli akamuoa na akawa naye. Lakini Mungu hakupenda, akaahidi kumuadhibu Daudi. Daudi hakung’ang’ania kuomba msamaha kupitia Nathani, ambaye alikuwa ni nabii ambaye Bwana alikuwa anamtumia kuwasiliana na Daudi wakati ule. Daudi aligeukia ukutani akamlilia Bwana hadi mahusiano yake na mkewe mpya Bathsheba, yakakubaliwa na Bwana. Tusome wote hadithi hii kwenye kitabu kifuatacho


2Samweli 12:1-25
Ndipo Bwana akamtuma Nathani aende kwa Daudi. Naye akamwendea, akamwambia, Palikuwa na watu wawili katika mji mmoja; mmoja wao alikuwa tajiri, wa pili maskini.

 Yule tajiri alikuwa na kondoo na ng'ombe wengi sana;bali yule maskini hakuwa na kitu, ila mwana kondoo mmoja, mdogo, ambaye amemnunua na kumlea; naye akakua pamoja naye, na pamoja na wanawe; hula sehemu ya posho lake, na kukinywea kikombe chake, na kulala kifuani mwake, akawa kwake kama binti.

Hata msafiri mmoja akamfikilia yule tajiri, naye akaacha kutwaa mmoja wa kondoo zake mwenyewe au mmoja wa ng'ombe zake mwenyewe, ili kumwandalia yule msafiri aliyemfikilia, bali alimnyang'anya yule maskini mwana-kondoo wake, akamwandalia yule mtu aliyemfikilia.
Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa;naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma.

Basi Nathani akamwambia Daudi, Wewe ndiwe mtu huyo. Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nalikutia mafuta, uwe mfalme juu ya Israeli, nikakuokoa na mkono wa Sauli;
nami nikakupa nyumba ya bwana wako, na wake za bwana wako kifuani mwako; nikakupa nyumba ya Israeli na ya Yuda; na kama hayo yangalikuwa machache, ningalikuongezea mambo kadha wa kadha.

 Kwa nini umelidharau neno la Bwana, na kufanya yaliyo mabaya machoni pake? Umempiga Uria, Mhiti, kwa upanga, nawe umemtwaa mkewe awe mke wako, nawe umemwua huyo kwa upanga wa wana wa Amoni.Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako.Bwana asema hivi, Angalia, nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, nami nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili.Maana wewe ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua.

Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi.Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa.Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa.

Naye Nathani akaondoka kwenda nyumbani kwake. Basi Bwana akampiga yule mtoto ambaye mkewe Uria alimzalia Daudi naye akawa hawezi sana.

Basi Daudi akamwomba Mungu kwa ajili ya mtoto; Daudi akafunga, akaingia, akalala usiku kucha chini.

Nao wazee wa nyumba yake wakaondoka, wakasimama karibu naye, ili wamwinue katika nchi; lakini hakukubali, wala hakula chakula pamoja nao.

Ikawa siku ya saba, yule mtoto akafa. Nao watumishi wa Daudi wakaogopa kumwambia ya kuwa mtoto amekufa, maana, walisema, Angalieni, yule mtoto alipokuwa angali hai, tulisema naye, asitusikilize sauti zetu; basi hatazidi kujisumbua, tukimwambia ya kuwa mtoto amekufa?

 Lakini alipoona ya kuwa watumishi wake wananong'onezana, Daudi alitambua ya kuwa mtoto amekufa; basi Daudi akawauliza watumishi wake, Je! Mtoto amekufa?Nao wakasema, Amekufa.
Ndipo Daudi akainuka pale chini akaoga, akajipaka mafuta, akabadili mavazi yake; akaingia nyumbani mwa Bwana, akasali; kisha akaenda nyumbani kwake, na alipotaka wakamwandalia chakula, naye akala.

Watumishi wake wakamwambia, Ni neno gani hili ulilolitenda? Ulifunga na kulia kwa ajili ya mtoto, alipokuwa hai; lakini mtoto alipokuwa amekufa, uliinuka ukala chakula.
 Akasema, Mtoto alipokuwa hai, nalifunga, nikalia; kwa maana nalisema, Ni nani ajuaye kwamba Bwana atanihurumia, mtoto apate kuishi?Lakini sasa amekufa nifungie nini? Je! Naweza kumrudisha tena? Mimi nitakwenda kwake lakini yeye hatanirudia mimi.

Naye Daudi akamfariji Bath-sheba mkewe, akaingia kwake, akalala naye; naye akazaa mwana, akamwita jina lake Sulemani. Naye Bwana akampenda;
akapeleka kwa mkono wa Nathani, nabii, naye akamwita jina lake Yedidia, kwa ajili ya Bwana.

Tunaona katika mifano ndani ya masomo yaliyopita kwamba watumishi wa Mungu hawa walikuwa na mahusiano binafsi na Mungu na walimgeukia Mungu wao wenyewe hadi Mungu akabadilisha na kuigeuzia mbali hasira yake na kuwasamehe.

Usipende sana kutumia mtu wa kati ili kumfikia Mungu, Mungu yupo kwa ajili yako na anakusikiliza kila siku, kazi yako ni kumuomba na kumtumikia kwa uaminifu.

Waombaji wengi kwa sasa wamekuwa siyo waaminifu na dunia imejaa watumishi hewa kila mahali hivyo hautakiwi kutegemea mtu mwingine akuunganishe na Mungu. Mtu mwenye nafasi nzuri kabisa kuliko wote ya kusema na Mungu kuhusu maisha yako ni wewe mwenyewe.

Jenga mahusiano binafsi na Mungu ili nyakati zinapokuwa ngumu uweze kugeukia ukutani na kusema naye na kuyapata majibu yako mara moja.

FAIDA NYINGINE YA KUWA NA MAHUSIANO BINAFSI NA MUNGU

KUWEZA KUPATA NENO LA WAKATI
Katika kila hali unayopitia mpendwa lipo neno la wakati katika hali husika. Neno la wakati ni Mungu anasema nini kuhusu hali yako na siyo watu wanasema nini katika hali yako unayopitia kwa sasa. Ni muhimu sana kupata neno la wakati ili uweze kuwa na uelekeo utakao kufikisha mahali panapostahili. Wana wa Israeli waliweza kudai mfalme kwa sababu hawakuwa na neno la wakati ule, ambapo neno la wakati ule kutoka kwa Bwana lingewaambia dhahiri kwamba haukuwa wakati wa kutafuta mfalme.

Yuda naye alijinyonga kwa sababu hakupata kulijua neno la wakati. Utabiri ulikuwapo dhidi yake kwamba angemsaliti Yesu, lakini haupo utabiri juu yake kuwa atajinyonga. Alichofanya Yuda ni ‘kujiongeza’ mwenyewe bila kutafuta neno la wakati ambalo lingetoka kwa Bwana kuja kumuokoa katika saa ile. Huyu yeye alijikuta katika hali ambayo alikuwa amechanganyikiwa akaona “he was too bad to turn to God,” yaani alikuwa mbaya sana kiasi cha kutoweza kumgeukia Mungu. Hakuna nyakati kama hizo katika maisha yako mpendwa. Hakuna umbali utakaofikia ambao utakuwa ni mkubwa sana kiasi kwamba huwezi kumgeukia Mungu maadam bado uko duniani. Huwezi kumgeukia Mungu ukiwa umekufa tu; hapo ndo huna namna.

Neno la wakati katika shida ni neno la wokovu, neno la wakati katika vita ni amani na ushindi, ni maji katika kiu na chakula katika njaa na dawa katika maradhi. Hivyo katika maisha yako na katika kila hali unayopitia, lipo neno la wakati la kukupitisha hapo unapopitia na ni la ushindi na amani. Tafuta neno la wakati sasa, na ni Mungu pekee anayeweza kukupa neno la wakati wala siyo rafiki zako au mganga wa kienyeji. Kuwa na mahusiano binafsi na Mungu ndiyo njia pekee ya kujihakikishia neno la wakati katika kila hali unayopitia.

Lipo neno la wakati kwako wewe uliyeachwa na mchumba, liko neno la wakati kwako wewe uliyedharauliwa na kushindwa kuishi kwa amani na furaha. Liko neno la wakati hata kwako wewe unayetafuta kuolewa na hujapata mume wa kukuoa.

Lipo neno la wakati hata kwako wewe ambaye madaktari wamekwambia kwamba huo ugonjwa wako hauwezi kupona, lipo neno la wakati hata kwako wewe dada unayejiona huvutii kiasi cha kutosha kuwa na mume.

Lipo neno la wakati kwako wewe mama mjane, lipo neno la wakati kwako wewe uliyefiwa na watu uliowategemea, lipo neno la wakati kwa yatima na masikini wa kutupwa.

Lipo pia neno la wakati kwa wale wenye viburi na waliojawa na tamaa za dunia, lipo neno la wakati kwa wale wasiopenda kushaurika na wanaodhani wao ndo wao na hii dunia wameshaiweka viganjani.

Lipo neno la wakati kwa wapendwa wasiotaka kuwajali wengine kisa wao wameinuliwa na Mungu na hata kwa watumishi wa Mungu wenye majivuno na wanaong’ang’ania dhambi na fahari za kidunia zisizo za kimungu.

Lipo neno la wakati kwa wale waliotengwa na makanisa kwa kufanya dhambi zilizoonekana. Maana makanisani wanatengwa watu wanaofanya dhambi za kuonekana na wanaachwa wale wote ambao bado dhambi zao hazijaonekana hata kama ni kubwa kuliko zile zilizoonekana. Nao hao wafanyao dhambi zisizoonekana na watu lipo neno la wakati kwa ajili yao Haleluya!

Lipo neno la wakati kwako wewe dada uliyeambiwa kuwa ni mbaya, tazama Mungu analo neno juu yako maana ndiye pekee aliyekuumba na anajua kama wewe ni mbaya au la, usiwasikilize wanaokuambia, nenda kwa Mungu mwenye neno la wakati akwambie namna ulivyo mrembo!

Neno la wakati linapatikana tu kwa kugeukia ukutani na kukutana na Muumba ambaye halali wala hasinzii na macho yake yapo duniani kuwaangalia wamtafutao kwa bidii ili awatatulie mahitaji yao. Kama ambavyo msomi anahangaika na bahasha kutafuta kazi ndivyo ambavyo Mungu anahangaika duniani akibisha milangoni mwa watu wanaotafuta neno la wakati awahudumie! Haleluya… 
Anagonga toka mlango hadi mlango akiwa na maneno ya nyakati ya kila mmoja wetu, hata la kwako wewe unayesoma somo hili! Kazi yako ni kufungua tu na kulipokea neno lako.

Maana Mungu naweza tena kumfananisha na muuza samaki au muuza bidhaa anayetembea mtaani akitangaza samakiii! Unachotakiwa wewe ni kumuita tu na anakupatia bure kabisa! Haleluya!
Wakati nikiwa advance nilikuwa nakaribia kufanya mtihani wa kidato cha sita, mama yangu mzazi alifariki dunia. Ugonjwa uliomuua ulikuwa ni kansa na nilimshangaa Mungu sana. Unajua wakati huo Mungu alikuwa yupo karibu na mimi kwa namna ya ajabu sana na kitu cha mama yangu kufariki ni kitu ambacho kilinishitua sana maana sikukitegemea hata kidogo. Hii ni kwa sababu Mungu alikuwa amenitumia pamoja na watenda kazi wa Fimbo ya Musa kufungua magonjwa ya kila aina, kupitia sisi wenye kansa walikuwa wanapona, wenye uvimbe tumboni, wenye appendix walikuwa wote wanafunguliwa hapohapo tunapoomba.

Lakini katika suala la mama tulikuwa tumeomba mara kadhaa bila mafanikio. Tulipoamua siku moja kwenda kukutana na mama ana kwa ana ili tumuombee, tulifika nyumbani na tukakuta umati wa watu wenye huzuni na maombolezo, kaka yangu aliangua kilio na kuniambia kuwa nilikuwa nimefika tu na mama anafariki. Sikumuelewa Mungu kabisa.

Wakati huo ulikuwa ni mwezi mmoja tu kabla ya kufanya mtihani wa form six na nilikaa siku nne tu za maombolezo nikarudi shule. Watu waliosikia habari za msiba ule na yaliyonipata-wanafunzi wenzangu walikuwa wanaogopa kukutana na mimi kwani walijua kuwa hali yangu ilikuwa mbaya sana na walidhani pengine ningekuwa nalia muda wote.

Siyo wao tu, hata mimi mwenyewe nilifikiri kuwa nikisharudi shule ningekuwa na muda mwingi sana wa kulia kuliko kufanya jambo lingine lolote. Cha ajabu ni kwamba tangu siku niliyoondoka nyumbani hadi siku niliyofanya mtihani; sikuwahi hata kulengwa na machozi kuhusu suala la mama. Hii ni kwa sababu Mungu hakuniacha katika wakati husika na aliniletea neno la wakati kupitia ndoto.

Siku moja nikiwa nimelala nilijikuta ndotoni niko nimekaa na mtu kama ambavyo mtoto anavyopakatwa na baba yake, nilimlilia mtu huyu ambaye nafsi yangu ilikuwa imeongozwa kuwa ni Mungu, naye alikuwa akinifariji na kuniambia maneno ya kunibembeleza kuwa alielewa hali yangu na jinsi nilivyoumia na alikuwa ana mawazo mema na mimi na kamwe hataniacha.

Nililia sana kwenye ile ndoto, na hatimaye ndoto iliisha na nikawa na amani tangu pale hadi watu waliokuwa wananiona wakawa wanakiri mbele yangu kuwa walikuwa wanashangazwa jinsi nilivyokuwa na moyo uliochangamka katika kipindi kigumu kama kile.

Ashukuriwe Mungu ambaye alijua kuwa nilikuwa nahitaji neno la wakati na hii ni kwa sababu nilikuwa na mazoea ya kugeukia ukutani na kukutana naye moja kwa moja kwanza kabla sijamsikiliza mtu mwingine yeyote kuhusu hali husika.

Umeona sasa? Neno la wakati ni kila kitu katika maisha yako. Neno la wakati ndiyo dira na kila mtu analihitaji. Geukia ukutani sasa utafute neno la wakati. Yule alijinyonga na yule mwingine alikunywa sumu kwa sababu alikosa neno la wakati.


Usikose kuendelea na mfululizo huu wa somo la kugeukia ukutani katika sehemu zinazofuatia. Waalike wengine wasome masomo haya kwa kusambaza.

No comments:

Post a Comment