Monday, October 31, 2016

OMBA MUNGU AKUPE HEKIMA YA KUISHI WAKATI WA NEEMA



“Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa” (TITO 2:11)
 Bwana wetu Yesu Kristo apewe sifa na utukufu daima!

Utangulizi
Ninamshukuru Mungu aliyeweka somo hili moyoni mwangu na kunipa mwongozo wa kukushirikisha siri hii ya pekee. Somo hili linalenga kukupa ufahamu wa nyakati tulizopo sasa (katika ulimwengu wa roho) na namna inavyokupasa wewe kuishi ndani yake ili ufaidike na baraka za wakati huu. Somo hili ni mwendelezo wa masomo ambayo Mungu amekuwa akinipitisha binafsi juu ya umuhimu wa kutambua majira na nyakati zinazopita kwenye maisha ya mtu ili aishi sawasawa na mapenzi ya Mungu kwenye nyakati hizo. Kitabu cha Luka kinatupa picha ya madhara yanayoweza kutokea pale ambapo mtu/watu hawana hekima juu ya muda waliopo na namna muda huo ulivyobeba maisha yao. Biblia inasema:

Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, akisema, Laiti ungalijua, hata wewe katika siku hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua majira ya kujiliwa kwako. (Luka 19:41-44)

Katika habari hiyo hapo juu, Yesu anaeleza mambo ambayo yataupata mji wa Yerusalemu katika siku za usoni. Anasema unakuja wakati ambapo mji huo utazingirwa na adui zake na kuuteka. Watauangusha mji pamoja na watu walio ndani yake, wasiache chochote kilichosimama. Lakini anasema haya yote yataupata mji kwa sababu haukutambua majira ya kujiliwa kwake. Sasa ukiusoma huo msitari wa 44 katika tafsiri ya Amplified Bible utagundua kuwa wakati unaozunguziwa hapa ni wakati ambapo neema ilikua imeachiliwa juu ya mji kwa ajili ya wokovu lakini watu wa mji huo hawakutambua. Amplified Bible inasema:

“And they will dash you down to the ground, you [Jerusalem] and your children within you; an they will not leave in you one stone upon another, [all] because you did not come progressively to recognize and know and understand [from observation and experience] the time of your visitation [that is, when God was gracious toward you and offered you salvation through Christ].” Luke 19:44 (AMP)

Kwa tafsiri hii ya Amplified Bible tunapata kujua kuwa madhara yatakayoupata mji huu wa Yerusalemu yanatokana na tatizo moja tu – kutokujua/kutokuelewa/kutokutambua wakati ambapo Mungu alikuwa ameachilia neema yake kupitia Yesu Kristo kwa ajili ya mji kuokolewa. Sasa utaelewa ni kwa nini Mtume Paulo anaweka msisitizo mkubwa katika suala la kutambua muda/majira. Ndani ya nyaraka zake mbili tofauti, Mtume Paulo anasisitiza jambo hili la kutambua wakati japo yeye anatumia lugha ya kuukomboa wakati:

Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. (Waefeso 5:15-16)
Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati. (Wakolosai 4:5)

Jumla ya mambo yote haya ni kuwa: muda/wakati ni jambo la kiroho na Mungu anataka watu waishi kwa hekima sana kutegemea na wakati waliopo. Pia, kwa kuwa muda ni (temporal) basi lazima uelewe kuwa mambo yaliyobebwa kwenye muda hutoweka pale muda wake unapokwisha. Nataka kukwambia kuwa katika vitu ambavyo shetani anafurahi sana kuviona ni pamoja na kuona watu wa Mungu wanaishi pasipo kutambua wakati waliopo. Somo hili linataka kukutoa hapo!

Neema ni kipindi maalumu

Nimemwomba Mungu anisaidie namna ya kukueleza jambo hili kwa namna ambavyo utaelewa. Kama utakuwa na maswali juu ya eneo hili tafadhari usisite kunitafuta kwa simu au email, au whatsapp au facebook.

Neema ni kitu anachopewa mtu pasipo kusitahili. Ni upendeleo maalumu kutoka kwa mtu atoaye kwenda kwa anayepewa. Mtume Paulo ametusaidia kuelewa maana ya neema kwa kutumia mfano wa mtu anayefanya kazi na yule asiyefanya kazi. Anasema:
Lakini kwa mtu afanyaye kazi, ujira wake hauhesabiwi kuwa ni neema, bali kuwa ni deni. Lakini kwa mtu asiyefanya kazi, bali anamwamini yeye ambaye amhesabia haki asiyekuwa mtauwa, imani yake mtu huyo imehesabiwa kuwa haki. (Warumi 4:4-5)

Paulo anasema kuwa ujira/mshahara wa mfanya kazi hauwezi kuitwa neema – bali ni deni – kwa sababu kila mtenda kazi amestahili ujira wake (1 Timotheo 5:18). Lakini, kwa mtu ambaye hajafanya kazi ila akahesabiwa kuwa amestahili kuwepa ujira/mshahara basi ule ujira wake sio deni bali ni neema. Naamini tunaenda pamoja!

Sasa Biblia inatuambia kuwa Kristo alipokuja alileta neema! Oooh hii ni habari njema. Yohana 1:17 inasema: Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo. Kwa hiyo katika mkono wa Yesu Kristo iko neema na kweli. Sasa kama neema ni kitu unachopewa pasipo kusitahili na mkononi mwa Yesu iko neema, hii inamaanisha kuwa mkononi mwa Yesu viko vitu vingi ambavyo tunaweza kuvipata ambavyo kwa kawaida hatukustahili kuvipata.
Bibia inasema jambo la kutia moyo sana katika Tito 2:11, inasema: “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa”. Neema imefunuliwa. Haleluya haleluyaa!!

Huu msitari wa Tito 2:11 una jambo la ajabu sana ambalo ndilo limebeba msingi wa somo hili. Paulo anasema “neema … imefunuliwa”. Hili linatupa kujua kuwa neema hii ilikuwepo tangu zamani … lakini ilikua haijafunuliwa. Ndiyo! Tangu Adamu na Hawa waasi pale bustanini, neema iliachiliwa lakini haikufunuliwa. Watu wa agano la kale walitembea chini ya kipindi ambacho neema ilikuwepo lakini ilikua imefichwa (Waefeso 3:1-5). Sisi watu tuliofikiwa na zamani hizi tunaishi kwenye kipindi ambacho neema imefunuliwa.

Roho mtakatifu alinishirikisha siri hii ya ajabu siku moja nikiwa katikati ya maombi. Nilisikia sauti ya Roho Mtakatifu akiniambia:
Ijapokuwa neema imefunuliwa bado watu wengi hawataweza kufaidika nayo kwa sababu hawajatambua nyakati zilizopo. Ndani ya neema kuna kila kitu unachokihitaji pasipo kuhitaji wewe uhangaike kutafuta kwa sababu unapewa chini ya neema iliyopo. Lakini ipo hekima inayohitajika ili mtu aweze kunufaika na wakati wa neema – akiikosa hiyo hekima mtu huyo atakosa faida zote zinazopatikana kwenye neema.

Neema ni kipindi maalumu! Kuna kipindi neema haikuwepo kabisa. Kuna kipindi neema ilikuwepo lakini ilikua haijafunuliwa. Sasa hivi ni kipindi ambacho neema imefunuliwa. Kuna kipindi kinakuja ambapo neema itaondolewa.

Nilimwomba Roho Mtakatifu anipe mfano rahisi wa kuelewa jambo hili. Akanirudisha kwenye Kitabu cha Mwanzo kwa habari ya Yusufu na ndoto ya Farao:
Ikawa, mwisho wa miaka miwili mizima, Farao akaota ndoto; … Hata asubuhi roho yake ikafadhaika; akapeleka watu kuwaita waganga wote wa Misri, na watu wote wenye hekima walioko. Farao akawahadithia ndoto yake, wala hakuna aliyeweza kumfasiria Farao mambo hayo … Yusufu akamwambia Farao, Ndoto ya Farao ni moja; Mungu amemwonyesha Farao atakayoyafanya hivi karibu… Tazama, miaka saba ya shibe inakuja, katika nchi yote ya Misri… Kisha kutakuja miaka saba ya njaa baada yake; na shibe ile yote itasahauliwa katika nchi ya Misri, na njaa itaiharibu nchi. (Mwanzo 41:1, 8, 25, 29, 30)

Ukipata nafasi soma sura hii ya 41 yote. Ila ninachotaka uone hapa ni kuwa Farao aliota ndoto juu ya miaka saba ya shibe na miaka saba ya njaa iliyokuwa inakuja katika dunia. Jambo la kujua ni kuwa hayo majira yaliyokuwa yanakuja juu ya nchi Misri yalikuwa yanakuja juu ya dunia yote hadi kule alikuwa anaishi mzee Yakobo – baba yake Yusufu.

Farao alipata neema ya kuambiwa juu ya majira na nyakati zilizokuwa zinakuja katika dunia. Watu wa mataifa mengine hawakuambiwa. Miaka saba ya shibe ilipokuja dunia yote ilikua na chakula cha kutosha ndio maana huoni mataifa mengine yakienda Misri kununua chakula kwenye miaka hiyo ya shibe. Ni kwa sababu neema ilikua imeachiliwa kote. Kila mahali palikua na chakula cha kutosha. Hata wale ambao walikua hawajui majira waliyopo bado walinufaika na neema iliyokuwepo.

Lakini kwa Misri wao walikuwa na ajenda ya ziada. Walikuwa wamepewa hekima ya kuishi kwenye wakati huo wa neema. Wao waliutumia wakati wa neema kujiwekea akiba ya kutosha kwa ajili ya wakati wa baadae. Baada ya miaka saba – neema ikaondolewa!

Neema ilipoondolewa, iliondolewa kwa mataifa yote – sio Misri tu! Sasa kila taifa ambalo halikupata hekima ya kuutumia wakati ule wa neema likaanza kupata shida ya chakula. Mataifa yote yakaenda Misri kununua chakula. Ila jambo la kushangaza ni kuwa hata wamisri wenyewe ambao nchi yao ilipewa hekima ya kuweka akiba bado na wao hawakuweka akiba! Unasema nimejuaje? Biblia inasema hata Wamisri wenyewe walienda kununua chakula kwa Yusufu! (Mwanzo 41:55).

Ninachotaka uone hapa ni kuwa neema ikiachiliwa inaachiliwa kwa watu wote, lakini ni watu wachache sana wanaopata hekima ya kuitumia hiyo neema kwa ajili ya maisha yao ya baadae pale ambapo neema itaondolewa. Watu wengi wanafikiri kuwa neema itakuwepo siku zote! La hasha! Neema ni kipindi maalumu! Kuna wakati lazima neema iondolewe na huo ndio wakati ambao watu wengi huwa wanaingia katika shida kubwa – kwa sababu hawakutambua majira ya kujiliwa kwao.

Ndio maana watu wawili wanaweza kuokoka wote katika siku moja – wakiwa kwenye (level) sawa ya kimaisha. Lakini baada ya muda mfupi unaona mmoja wao amefanikiwa na anazidi kusonga mbele kwa mafanikio kuliko mwenzake. Je, tatizo liko wapi? Tatizo liko kwenye namna wanavyotumia neema waliyoipata walipookoka. Kuokoka kunakupa (access) ya kuingia kwenye bank account ya neema iliyo ndani ya Kristo Yesu. Lakini kama huna hekima ya kutumia fursa hiyo, bado kuokoka hakuwezi kubadili maisha yako – hata kama neema ipo.

Chukua hatua ya kuomba hekima

Kila mtu kwenye dunia hii ana wakati wake wa neema. Kuna kipindi ambacho Mungu amekubariki sana au atakubariki sana. Watu wengi huwa wakiwa kwenye kipindi hiki cha mafanikio huwa wanasahau na kufikiri kuwa kipindi kama hiki kitaendelea tu siku zote. Hapana! Biblia inasema pamoja na kuwa na wakati wa kucheka na kufurahi lazima pia uje wakati wa kulia (Muhubiri 3:4). 

Namna gani una hekima ya kutumia wakati wako wa kucheka ndio itakusaidia namna utakavyoishi wakati wa kulia. Omba hekima ya Mungu kukusaidia kutambua majira uliyopo sasa na akusaidie kujiandaa kwa ajili ya nyakati ngumu zinazokuja.

Nataka kusisitiza jambo moja kabla sijahitimisha. Yesu alipokuja duniani alituletea neema. Ndani ya neema ya Yesu kuna (package) kubwa sana ya baraka za Mungu kwetu sisi. Lakini tunaweza kushindwa kunufaika nazo kwa kukosa hekima na maarifa ya kuitumia hiyo neema. Kumbuka Mungu anasema “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa” (Hosea 4:6).

Kuna maarifa ya ki-Mungu ambayo inahitajika kuweza kuishi wakati wa neema. Japokuwa wengi tunajua kuwa neema ya Yesu imeachiliwa bado hatuna hekima ya kutusaidia kuitumia neema hiyo. Ndiyo maana bado shetani anatuonea, magonjwa yanatusumbua, umaskini umetujaa, hatufanikiwi kwa lolote tunalolifanya licha ya kwamba tumeokoka. Hapana! Neema ya Yesu imekuja ili tufaidike wakati huu na kwa ajili ya wakati ujao. Watu wa Misri walijulishwa wakati wa neema na wakati wa mabaya lakini bado hawakuweza kuitumia neema ile kujiwekea akiba ya chakula kwa ajili ya wakati wa njaa.

Hapana! Tusiwe kama hao. Chukua hatua ya kupiga magoti na kuomba Mungu akupe hekima ya kuitumia neema iliyofunuliwa ndani ya Kristo Yesu. Kumbuka kuwa Mungu anafurahishwa na mafanikio ya watu wake (Zaburi 35:27); lakini pia yeye anatuwazia mawazo mema wala si ya mabaya (Yeremia 29:11). Njia mojawapo ambayo Mungu anaitumia katika kutufikisha kwenye mema aliyokukusudia, ni kwa kukupa hekima ya kuishi wakati ambao neema imefunuliwa.

Mungu akubariki sana!
Mwl. Lukiko

No comments:

Post a Comment